Ilipoishia 

Caren alisimama baada ya kuniona simjibu alichokua akinisemesha, nilianza kuhema kwa kasi,  hofu ilikua imenitawala vya kutosha. 

“Kuna nini Celin?” aliniuliza, nilimjibu Caren kwa sauti ya chini iliyojaa hofu na mtetemo wa  Uwoga uliopitiliza. 

“Kuna Mtu nyuma yetu” Nilitamani kulia kwa jinsi woga ulivyokua umenishika, Caren aligeuka  nyuma kisha akarejesha macho kwangu. Akaangua kicheko na kuanza kuongea kama mlevi . Endelea

SEHEMU YA PILI

“Kumbe umekunywa pombe Celin, Ha!ha! Hakuna Mtu. Ulisema hautumii pombe mbona  umelewa ha!ha!ha!” Haraka niligeuka nyuma, hapakua na yeyote yule, lakini hisia yangu ya  ndani iliniambia yule Mzee analifahamu jambo fulani kuhusu nyumba yetu. Nilitabasamu ili tu  kumfanya Caren aamini kua nilikua nimelewa kidogo. 

Tuliporudi ndani tulikuta Watu wakiendelea na tafrija hiyo fupi, baadaye mishale kama ya saa  tano hivi walitawanyika na kutuacha Wana Familia pekee, Mimi, Baba na Mama. Kwakua Usiku  ulikua mwingi, Baba akatuambia tukalale, asubuhi tutafanya kazi ya kuweka mazingira sawa.  Mimi niliingia chumbani kwangu, chumba changu kilikua juu. 

Baada ya kuingia chumbani nilijikuta nikiendelea kufikiria hatua za yule Mzee, bahati nzuri  dirisha langu lilikua likiitazama vizuri nyumba ya yule Mzee, nilisogea taratibu hadi dirishani  kisha nilichungulia, palikua kimya sana. Hapakua na dalili ya Mtu yeyote yule, nilisimama hapo  kwa zaidi ya dakika kumi lakini sikuambulia chochote kile. 

Nilikata shauri nikaingia bafuni kuoga kisha nilipomaliza nilirudi kitandani na kupumzika. *** 

Nilichokiona, nilichokihisi kilibakia ndani yangu. Sikupenda kuwaingiza wazazi wangu kwenye  presha ya aina yoyote ile, kama ukweli nitautafuta mwenyewe. 

Siku iliyofuata ilianza kwa baridi kali sana, nilipaswa kuelekea chuoni. Nilijiandaa, baada ya  dakika kama kumi nilikua tayari kwa ajili ya kuondoka na kuelekea chuoni. 

Niliwaaga wazazi wangu kisha niliondoka. Nilipofika nje nilipata wazo la kubadilisha njia,  niligeuka na kuelekea upande wa nyumba ya yule Mzee, mara zote nyumba yake ipo kimya.  Hapasikiki sauti ya aina yoyote ile, nilipiga hatua zangu za taratibu nikiwa nimevalia viatu virefu  kama buti hivi, suruali nyeusi na shati jekundu kisha koti la kunikinga na baridi. 

Nafsi yangu ilizidi kuniambia kua kuna jambo napaswa kulijua kuhusu nyumba yetu mpya, Mtu  pekee ambaye alionesha hisia ya kujua jambo alikua ni huyu Mzee wa ajabu. Basi, nilipofika  aneo la geti lake niliona pameandikwa ‘Mwanzo wa Mwisho’  

“Mwanzo wa Mwisho?” niliyarudia maandishi yaliyopo getini, nilihema. Yalikua ni maneno  magumu kiasi kwamba sikuelewa chochote kile, hisia mbaya dhidi ya huyu Mzee ilichipua zaidi  ndani yangu. Wakati huo jua lilikua likianza kuchomoza kwa mbali, palikua na mwanga wa  kutosha, upepo wa hapa na pale. 

Niligeuka kuangalia nyumbani kwetu, kisha nilitazama tena pale getini, sikupata tafsiri ya haraka  haraka juu ya yale maneno. Nilimeza funda zito la mate, nilitazama saa yangu, ilisoma ni saa  2:13 Asubuhi. 

Niliona bado nina muda wa kutosha kabla ya kuelekea chuoni pengine naweza kuzungumza na  yule Mzee angalau nipate ufumbuzi wa maswali magumu yaliyojaa kichwani pangu. Nilisita-sita  lakini niliweza kugonga geti

Palikua kimya sana kama sehemu isiyotembelewa na Mtu kabisa. Niligonga tena, nikagonga  zaidi kwa kutumia mkono wangu wa kushoto huku nikisema 

“Kuna yeyote?” nilikua makini sikutaka wazazi wangu wajue chochote kile, palikua kimya sana.  Nilikata tamaa, sikuona dalili ya kufunguliwa Geti hilo dogo. Nililipa mgongo lile geti kisha  niliondoka hapo, nikasogea Barabara kuu nikapanda treni iliyokua ikielekea katikati ya Jiji, huko  ndiko nilikokua ninasoma. 

Niliketi siti namba 25, kando yangu alikuwepo Bibi mmoja. Nilimsalimu kwa heshima sana,  baada ya treni kuondoka aliniuliza 

“Kuna jambo linakutatiza?” sijui aliweza vipi kujua kua nilikua natatizwa na jambo fulani,  niliachia tabasamu kiasi ili kumjibu yule Bibi.  

“Kiasi, hata hivyo ni jambo la kawaida” nilimjibu, hakusema chochote. Alikaa kimya nami  nilikaa kimya nikisubiria kusikia angesema nini lakini aliendelea kukaa kimya. Dakika kama  kumi hivi, yule Bibi akaniambia 

“Nashuka kituo kinachofuata, kua makini sana Mjukuu wangu. Unakaribia kupoteza Watu  uwapendao kwa mpigo, kua jasiri. Wakati mwingine Maisha yanatupeleka shimoni makusudi”  Moyo wangu ulilipuka mithiri ya Volkano, simjui yule Bibi. Aliwezaje kuongea maneno mazito  kiasi kile, Watu niliowapenda sana walikua ni Wazazi wangu 

“Samahani unasemaje?” nilimkujia sura yangu, aliachia tabasamu tu akaniambia 

“Huwezi kuwaokoa, Hatma imewafikia” maneno yake yalikua mazito sana, kiasi kwamba  yalinifanya nilegee mwili mzima. Nilihisi ganzi moyoni mwangu, huzuni na hisia ya hasira.  Nikiwa ninaendelea kuyarudia maneno yake, mara treni ilikua imefika kituoni, yule Bibi  alishuka kisha alisimama akinipungia mkono wa kuniaga. 

Moyo uliniuma sana, hata safari yangu ya kuelekea chuoni niliiona kua ilikua nzito sana. Hapo  hapo nikaitoa simu yangu kwenye begi nikampigia Mama yangu kumuuliza kama walikua  salama. Mama alinitoa hofu, hata sauti yake ilionesha palikua shwari kabisa. 

Pumzi niliyoishusha ilikua kubwa, ilishuka kama gia ya gari. Kifua kilikua kizito, presha siyo  presha, yale maneno yalikua yanazidi kunipigia kelele masikioni mwangu. Ndani ya siku mbili  nilikutana na mauzauza ya kutisha, nilipiga moyo konde nikiamini hakuna anayeweza kuijua  hatma ya Mtu mwingine isipokua Mungu pekee. 

Nilipofika chuoni, nilikua na maswali mengi kichwani. Nilijiinamia kwenye meza, nilihisi kama  nilikua nimebeba mzigo mzito sana kichwani mwangu. Nikiwa hapo alikuja Caren, akanifanyia  utani ambao haukua kipaumbele kwangu 

“Una shida gani Celin?” aliniuliza, niliweka mikono yangu usoni, nilitamani kumueleza Caren  lakini sikupata ujasiri wa kufanya hivyo. 

“Celin, niambie una tatizo gani?” aliniuliza tena, bado nilikua kimya nikimwangalia. 

“Jana usiku ulikua hivi, unanificha kitu. Hata hivyo nimepewa hii barua nikupatie” Nilishtuka  kidogo 

“Imetoka wapi?”  

“Nimepewa na Bibi mmoja hapo nje amesema nikupatie wewe” Nilishtuka sana, niliogopa kisha  nilikimbilia nje ya geti la chuo, nilitazama huku na kule kama ningemwoma huyo Bibi, nilikua  na uhakika huwenda ni yule Bibi niliyekutana naye kwenye Treni muda mchache uliopita. Mara  Caren alifika 

“Sikuelewi Celin, kuna nini?” aliniuliza, nilimsogelea nikiwa nina hisia ya hofu na Mashaka  makubwa. 

“Yupoje?” 

“Mwembamba, amevaa koti la suti lililochakaa. Gauni la bluu, halafu amevalia raba chini” sifa  alizozitaja Caren zilifanana na sifa za yule Bibi niliyekutana naye kwenye treni. 

“Caren kuna kitu hakipo sawa, nilikutana na huyo Bibi kwenye treni. Ameongea maneno ya  kutisha sana, nipe hiyo Barua” Haraka Caren alinipatia Barua kisha niliifungua haraka,  nilikutana na karatasi nyeupe iliyoandikwa jina moja ‘ZENA’ 

“Zena” nilisema kwa hofu, nilirudi nyuma nyuma nikiwa nina hofu hadi pale nilipofika mwisho  nikakutana na ukuta wa uzio wa chuo, Caren alisogea naye akiwa kwenye Mshangao mkubwa  sana. Jina la Zena liliandikwa kwa herufi kubwa na wino mwekundu. Chozi lilikua linanitoka  huku ile kauli kua nitapoteza niwapendao kwa Mpigo ilikua ikijirudia akilini mwangu. 

Zena ni rafiki yetu, tokea nimefika chuo sikumwona. Nikamuuliza Caren 

“Umemwona popote?” 

“Nani?” 

“Zena” 

“Hapana, nilijaribu kumpigia nilipofika chuo lakini simu yake ilikua ikiita tu. Hebu niweke wazi  kuna nini?” Caren aliniuliza kwa hofu huku akiweka mikono yake kichwake pake, alikua njia  panda nami sikua na muda wa kumweleza zaidi. 

“Twende kwake Caren, tafadhali twende” nilisema huku chozi likizidi kunibubujika. Nilikua na  uchungu moyoni mwangu, nilianza kuwa na wasiwasi kua kuna jambo lililomfika zena. Maneno  ya yule Bibi yalizidi kujirudia akilini mwangu. Nilisimamisha Taxi haraka, tuliingia kwenye Taxi  huku Caren akinilazimisha niseme kinachoendelea, nilikua ninalia tu.

“Sasa Celin, usiposema nitajua nini. Yule Bibi ni Nani yako, kwanini amekutumia Barua yenye  jina la Zena?” aliniuliza Caren alikua amejawa na hofu, wasiwasi kwa pamoja. Niligeuka  kumtazama huku chozi likinibubujika  

“Sali, lisimfike lolote. Dunia inanigeuka Caren” nilisema kwa Uchungu, sikuweza kuongea  zaidi. Nilihisi uzito uliopitiliza, nilihisi kuchanganikiwa huku sura na maneno ya yule Bibi kizee  yakizidi kuendelea kutembea kichwani kwangu.  

Zena alikua anaishi kilomita chache kutoka pale chuoni, wastani wa nusu saa tulikua  tumeshafika mahali alipokua amepanga. Niligonga geti kwa nguvu kisha tulisubiria kwa sekunde  kadhaa kisha geti lilifunguliwa na Mama mwenye nyumba. 

Alionesha tabasamu mbele yetu sababu alikua akitufahamu, tulikua tukienda hapo mara kwa  mara lakini safari hii hakuna aliyerudisha tabasamu. Tulimpita kama wanariadha wa mbio ndefu  za Marathon, breki tulifunga mlangoni kwa Zena 

Tulisimama kwa sekunde kadhaa za kuhesabu, mlango ulionekana kua wazi sababu palikua na  upenyo mdogo. Tulitazamana, sura ya Caren ilijaa maswali mengi yasiyo na Majibu, sikuweza  kumweleza chochote kile hadi muda huo. 

Nilipopiga hatua kuusogelea mlango, Caren alinishika mkono akaniuliza 

“Nini kinaendelea Celin?” Alianza kuniuliza kwa sauti ya chini iliyojaa kilio cha hisia kali ya  hofu na woga kwa pamoja. Ni kama Caren alikua amenielewa, nilitikisa kichwa kumdhihirishia  kua Zena alikua shidani. Chozi lilikua likitububujika, nyuma yetu alifika Mama mwenye nyumba 

“Mabinti, kuna nini?” aliuliza yule Mama Mtu mzima, ndiye mmiliki wa nyumba ambayo Zena  alikua amepanga kwa ajili ya masomo ya Chuo. Niligeuka kumtazama huku chozi likinibubujika,  naye Mama akautazama Mlango wa Zena, akiwa kama Mtu mzima alikua ameelewa kua Zena  alikua matatizoni na pengine alikua ameshakufa.  

Macho yake pia yalimlenga kwa Mchozi. Nilielekeza macho yangu mbele kisha niliufungua  mlango taratibu, nikautosa mguu wangu ndani ya chumba, nilichokiona kilinifanya nipige yowe  kali la kuchanganikiwa. 

Kila mmoja wetu aliingia kushuhudia kile ambacho macho yangu yalikuwa shuhuda wa kwanza.  Zena alikua akining’inia kwenye kitanzi cha Khanga kilichofungwa kwenye feni, alikua  akizungushwa huku na kule kama Mzigo usio na thamani tena, ama kweli utu wa Mtu ni uhai  wake 

Zena alikua amekufa muda mrefu sana, binafsi nililia kwa uchungu sana. Mama mwenye  nyumba akakimbilia kumwita Mjumbe na mwenyekiti wa Mtaa. Bila hata kutumia vipimo  walithibitisha kifo cha Zena, rafiki aliyenipokea chuoni na kunifundisha Maisha ya Chuo jinsi  yalivyo.

Tulipishana Mwaka mmoja wa kuingia chuoni, alinitendea wema kila nyakati. Hata wakati  ambao alipaswa kufurahi alinipa furaha yake na kisha yeye alibakiwa na huzuni yangu.  Nilimwona akiwa anafunguliwa kutoka juu ya feni akiwa amevalia gauni lake jekundu. 

Hakika maneno ya yule Bibi yalianza kutimia, nilimpoteza mmoja nimpendaye. Nilijiegemeza  ukutani nikilia kwa kwikwi nikiushuhudia mwili wa Zena ukiondolewa na Askari Polisi  waliokua hapo baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Mwenyekiti wa Mtaa. 

Nini Kitaendelea? Usikose Sehemu Ya TATU 

COMMENTS ZIWE NYINGI SASA 

JIUNGE NA KIJIWENI WHATSAPP CHANNEL Kwa Kugusa Hapa 

Soma Riwaya Nyingine Za Kijiweni Kwa KUGUSA HAPA

Wewe kama MFANYABIASHARA.. Kuna wakati unatamani kuwafikia watu wengi zaidi na hujui wapi pa kuanzia , USIJALI kwani hapa ndipo ambapo MTAA UNAONGEA na tuko tayari kukusaidia kuwafikia watu wengi kwa BEI YA OFA

Njoo Utangaze Nasi Sasa Kwa Kutuambia Una TANGAZO Gani na unataka kutangaza kwa muda gani kwa kutuma ujumbe hapa WwhatsApp Kupitia Namba +255760871896 

Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx Nyumba Juu Ya Kaburi xx

1 Comment

Leave A Reply

Exit mobile version